
Gumzo kuu linalotawala duniani kote hivi sasa ni hatua ya Iran na mataifa sita yenye nguvu za kijeshi na kiuchumi kufikia makubaliano mapema juzi kuhusu kudhibiti mpango wa Iran wa nyuklia, huku nchi hiyo ikifaidika kwa kupata unafuu wa vikwazo vilivyowekwa dhidi yake yapata miaka kumi iliyopita.
Makubaliano
hayo ambayo hayakutarajiwa yameishangaza dunia. Hakuna aliyetarajia
siyo tu kwamba Iran siku moja ingekubali kukaa meza moja na mataifa
yenye urafiki mkubwa na hasimu wake Israel kuzungumzia udhibiti wa
mpango huo, bali pia mataifa hayo ya Magharibi hayakutarajiwa kufanya
mazungumzo na nchi hiyo wala kuipunguzia vikwazo vya kiuchumi kabla
haijasitisha mpango huo, mbali na kulitambua rasmi ‘Taifa la Israel’
.
.
Itakumbukwa
kwamba mchakato uliofanikisha makubaliano hayo ulianza kama mzaha miezi
michache iliyopita kwa Rais mpya wa Iran, Hassan Rouhani kumpigia simu
Rais Barrack Obama wa Marekani akitaka kurudishwa kwa uhusiano wa
kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili zenye uhasama mkubwa tangu
wanamgambo wa Iran walipouteka Ubalozi wa Marekani nchini humo mwishoni
mwa miaka ya 70. Huo ndio ulikuwa mwisho wa uhusiano wa kidiplomasia
kati ya nchi hizo mbili hadi leo.
Pamoja
na baadhi ya Wamarekani kudai kwamba wito wa Rais Rouhani ulikuwa na
ajenda ya siri, Rais Obama aliutafakari kwa hadhari kubwa na kuwataka
wananchi wake kutoa nafasi kwa Iran kuthibitisha kama kweli ilikuwa na
dhamira ya kutafuta amani. Baada ya kuridhika kwamba Iran ilikuwa na
dhamira hiyo, aliyakutanisha mataifa sita yenye nguvu, yaani Marekani,
Ufaransa, Ujerumani, Russia, China na Uingereza na kuyashawishi kwa
pamoja kufanya mazungumzo na Serikali ya Iran.
Mazungumzo
yamekuwa yakifanyika mjini Geneva, Uswisi kwa wiki kadhaa na
makubaliano ya mwisho yalifikiwa mwishoni mwa wiki baada ya siku nne za
majadiliano. Makubaliano hayo yanachukuliwa kama hatua ya kwanza muhimu
kuelekea kuondoa wasiwasi wa dunia kuhusu mpango huo wa nyuklia, lakini
pia yanajumuisha udhibiti wa hali ya juu dhidi ya taifa hilo kujipatia
silaha za nyuklia.
Kwa
maana hiyo, Iran itasitisha urutubishaji wa kiwango cha juu cha madini
ya urani na itafaidika kwa kuachiliwa kwa dola 4.2 bilioni
zilizozuiliwa katika benki za kigeni, hivyo kuweza kuanza tena biashara
ya madini ya thamani, bidhaa zitokanazo na mafuta pamoja na vipuri vya
ndege.
Madini
ya urani yaliyorutubishwa yanaweza kutumiwa kuendesha vinu vya nishati
ya kinyuklia ambalo sisi tunadhani ndio hasa lengo la Iran, lakini pia
yanaweza kutumiwa kutengeneza bomu la nyuklia iwapo yatarutubishwa
zaidi.
Tunaipongeza
Serikali ya Iran na wananchi wake kwa jumla kwa kuchagua amani badala
ya vita katika Mashariki ya Kati ambapo umekuwapo uhasama mkubwa kati
ya nchi nyingi za Kiarabu dhidi ya Israel, hasa kuhusu ‘Suala la
Palestina’. Bila shaka kuzuka kwa vita katika eneo hilo lenye utajiri
mkubwa wa mafuta kungeiathiri dunia nzima kiuchumi na nchi maskini kama
Tanzania ndizo zingeathirika zaidi.
Israel
inamiliki silaha za nyuklia. Jambo la kushangaza ni kuwa, wakati dunia
ikifurahia makubaliano hayo, Waziri Mkuu, Benjamin Netanyahu amesema
makubaliano hayo ni ‘mabaya’. Msimamo huo unathibitisha madai kwamba
kiongozi huyo amekuwa akifaidika kisiasa kutokana na mgogoro wa nchi
yake na Iran.