Mbeya/Dar. Mkuu wa Shule ya Sekondari St Francis ya mkaoni Mbeya
iliyoshika nafasi ya kwanza kitaifa katika Matokeo ya Kidato cha Nne
yaliyotangazwa jana, Sista Flossy Sequira amesema kuwa alikuwa na
uhakika kwamba shule yake ingefanya vizuri kwenye mtihani huo, huku
akitaja siri ya mafanikio.
“Tumefurahishwa na matokeo licha ya kuwa
tulikuwa tunafahamu fika kuwa tutafanya vizuri kwa kuwa huo ndiyo
utamaduni wetu, tutahakikisha tunaendelea kushika nafasi hiyo kila
mwaka,” alisema Sista Sequira.
Alipotakiwa kueleza siri ya matokeo hayo kwa shule
yake kila mwaka, mkuu huyo wa shule alisema: “Siri kubwa ya mafanikio
hayo ni kumtanguliza Mungu kila siku na ushirikiano wa hali ya juu
uliopo kati ya walimu, wanafunzi na uongozi wa shule.”
Aliongeza kuwa umakini walionao wanafunzi wa shule
hiyo ni sababu nyingine ambayo huwarahisishia walimu wakati wa
kufundisha, hata wanapowatolea majaribio ya mara kwa mara.
Naye Mkuu wa Shule ya Wasichana ya Canossa ya Dar
es Salaam, iliyoshika nafasi ya tano Yvonne D’souza, alisema amefurahi
kuwa mwanafunzi aliyeshika nafasi ya tatu katika kumi bora ametoka
shuleni hapo, lakini alitarajia wangefaulu wanafunzi zaidi ya watatu
katika kundi hilo.
“Kufaulu ni kawaida yetu, sisi tunafuata viwango
vya elimu vinavyotakiwa. Mwaka huu nimefurahi kwa sababu wasichana ndiyo
waliofaulu zaidi, ninataka wapande, wawe juu, huu ni wakati wao,”
alisema D’souza.
Kwa upande wake Mkuu wa Shule ya Wasichana ya
Marian, Flora Mapunda, ambaye shule yake imetoa wanafunzi wanne bora
ikishika nafasi ya sita, alisema matokeo hayo hayakumridhisha sana kwani
alitegemea wanafunzi wengi wangefaulu zaidi.
Katika matokeo hayo yaliyotolewa na Baraza la
Mtihani la Tanzania na kutangazwa na Kaimu Katibu Mtendaji wa baraza
hilo Dk Charles Msonde, Sekondari ya St Francis imekuwa ya kwanza,
ikifuatiwa na Marian Boys ya mkoani Pwani, huku Feza Girls ya jijini Dar
es Salaam ikiwa nafasi ya tatu.
Katika shule hizo kumi bora, Sekondari ya Precious
Blood ya Arusha imekuwa ya nne, Cannosa ya Dar es Salaam imekuwa ya
tano, Marian Girls ya Pwani nafasi ya sita, Anwarite Girls ya
Kilimanjaro ipo nafasi ya saba.