KUMEIBUKA
hoja nyingi zikiwamo za kwamba iweje mawaziri ambao CCM iliwaita
‘mizigo’ wamerudishwa kwenye Baraza la Mawaziri ambalo lilifanyiwa
mabadiliko na Rais wa Jamhuri ya Muungano, DK Jakaya Kikwete Jumapili
Januari 19, mwaka huu na kutangazwa mbele ya waandishi wa habari na
Katibu Mkuu Kiongozi, Ombeni Sefue?
Hoja
hizo zimeibuka baada ya Sekretarieti ya CCM, Chini ya Katibu Mkuu wake,
Abdulrahman Kinana, akishirikiana na Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi,
Nape Nnauye na wa Siasa na Ushirikiano wa Kimataifa, Dk Asha-Rose Migiro
kufanya ziara ya siku 26 katika mikoa ya Ruvuma, Mbeya na Njombe
kuwanyooshea kidole baadhi ya mawaziri wasiowajibika katika kuondoa kero
za wananchi.
Sambamba
na hilo, mawaziri hao na wengine jumla yao saba waliitwa mbele ya
Kamati Kuu ya CCM iliyokutana mapema, Desemba mwaka jana, kuhojiwa
kutokana na utendaji wao wa kuondoa kero za wananchi kutoridhisha.
Katika
mwito huo, alikuwamo aliyekuwa Naibu Waziri wa Fedha na sasa ndiye
Waziri wa wizara hiyo, Saada Mkuya Salum kwa niaba ya Waziri wake, Dk
William Mgimwa, Mungu amweke mahali pema peponi.
Wengine
walikuwa Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Christopher Chiza;
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi; Dk Shukuru Kawambwa; Waziri wa
Utumishi, Celina Kombani, Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
(TAMISEMI), Hawa Ghasia; Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk Abdallah
Kigoda na Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Dk Mathayo David Mathayo.
Katika
kundi hilo, Waziri aliyeachia ngazi ni Dk Mathayo, ambaye ni kutokana
na tuhumu za Oporesheni Tokomeza Ujangili kutumiwa kinyume na malengo na
watendaji na kugeuza kuwa ya utesaji, ukandamizaji na ya vitendo
vingine vya kinyama.
Uteuzi
wake ukatenguliwa na Rais Kikwete pamoja na Waziri wa Mambo ya Ndani,
Dk Emmanuel Nchimbi; Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Shamsa
Vuai Nahodha. Huku Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Hamisi
Kagasheki akijiuzulu.
Kwenye
baraza hilo jipya, hao wanne wameondolewa pamoja na wengine, ambapo
kwenye Baraza hilo sura mpya kumi zimejitokeza na kuungana na mawaziri
wengine ambao chama kiliwaona hawawajibiki vizuri ipasavyo katika
kushughulikia au kutatua kero za wananchi.
Kutokana
na kutowajibika huko kulibainishwa na Sekretarieti ya Halmashauri Kuu
ya CCM Taifa inayoongozwa na Katibu Mkuu wake, Kinana ambayo tangu
kuundwa kwake mwanzoni mwa mwaka jana, imekuwa ikifanya ziara mikoani
kukutana na wananchi kusikiliza kero zao, kukagua utekelezaji wa ilani
ya uchaguzi ya CCM na kuimarisha chama mikoani.
Sekretarieti
hiyo imefanya kazi nzuri na kurudisha imani ya chama kwa wananchi,
lakini imefanya yote hayo kwa mujibu wa agizo la Mkutano Mkuu wa Taifa
wa Nane wa CCM uliofanyika Novemba 2012 mjini Dodoma, ambao ulikiagiza
chama, kiwe karibu na wananchi, kisikilize changamoto zao na kiwasemee
wananchi na hasa wanyonge.
Sekretarieti
imetekeleza azimio hilo na kusikiliza matatizo ya wananchi kwa kufanya
ziara nyingi, ikiwamo ya mikoa ya Ruvuma, Mbeya na Njombe ambapo
imefanya zaidi ya mikutano 121 na kusafiri zaidi ya kilometa 6,000
katika majimbo, wilaya na mikoa hiyo, ikizungumza na wananchi, mabalozi
na halmashauri za chama na kusikiliza kero zao.
Kutokana
na hoja hizo kuendelea kusambaa, hasa baada ya Baraza kutangazwa ambalo
ni hiari ya Rais kumteua au kutomteua yeyote, Katibu wa NEC, Itikadi na
Uenezi, Nape amezungumza na waandishi wa habari kuujulisha umma kwamba
chama hakikutaka kuwaondoa madarakani mawaziri hao, bali kilitaka
wajirekebishe upungufu wao.
"Haikuwa
hoja ya CCM kuwafukuza mawaziri hao bali kuchukua hatua za kurekebisha
upungufu... Kuwafukuza inaweza kuwa njia mojawapo ya kutatua tatizo
lakini sio njia pekee.”
“CCM
inaamini kwamba kurudishwa kwao mawaziri hao 'mizigo' wamepewa fursa ya
kurekebisha upungufu tuliosema kwa niaba ya wananchi. Chama kinaamini
kwamba mawaziri hao hawatajibweteka bali watatimiza wajibu wao na
kuhakikisha wanawatumikia wananchi ambao ndio waajiri wa Serikali.
"Chama
hakitasita kuchukua hatua kali dhidi ya mawaziri na watendaji wengine
watakaoshindwa kurekebisha upungufu na watakaoshindwa kutimiza wajibu
wao vizuri. Wakumbuke kushindwa kwao kutimiza majukumu yao ni hujuma kwa
Ilani ya uchaguzi ya CCM, CCM haitavumilia usaliti huo.CCM ikikaa kimya
itakuwa inajinyonga yenyewe jambo ambalo hatutaruhusu kabisa,"
amesisitiza.
Kauli
hiyo ya Katibu wa NEC, Nape inaonesha dhamira ya dhati ya CCM ya
kuhakikisha mawaziri hao wanatumia fursa adimu waliyopata kuwajibika,
kusikiliza kero za wananchi na kuwatembelea katika maeneo yao na
kuzungumza nao ili kujua shida zao.
Ni
ukweli usiopingika, Chama kikibaki kimya, wakati kilikuwa kimeanza
kurudi kwenye reli kama Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Mbeya, Godfrey Zambi
ambaye sasa ni Naibu Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, alivyokuwa
anasema kwamba Kinana anarudisha chama kwenye reli, kitatoka nje ya
mataruma na kufa kifo cha mende kama watendaji wa Serikali
hawatawajibika katika kuondoa kero za wananchi.
Kutokana
na mkakati huo wa kukirudisha chama kwenye reli, CCM haitasita
kuendelea kuchukua hatua kali ndani ya chama dhidi ya mawaziri na
watendaji wengine watakaoshindwa kujirekebisha na kuwajibika kutatua
kero za wananchi ambao ndio mtaji wa chama na Serikali.
“Chama
Cha Mapinduzi hakitasita kuchukua hatua kali dhidi ya mawaziri na
watendaji wengine watakaoshindwa kurekebisha mapungufu na watakaoshindwa
kutimiza wajibu wao vizuri,” anasema Nape.
Ni
ukweli usio na kipingamizi kwamba, kushindwa kwa watendaji hao kutimiza
majukumu yao ni hujuma kwa Ilani ya uchaguzi ya CCM, CCM haitavumilia
usaliti huo.”
Ili
CCM ibaki madarakani kuongoza dola, lazima watendaji wake wawajibike
kikamilifu kwa kusikiliza na kutatua kero za wakulima, wafugaji, wavuvi
na makundi mengine katika jamii, vinginevyo itakuwa vigumu chama
kushinda ushindi wa kishindo.
Nafasi
hiyo adimu waliyopewa mawaziri, japo imebaki miezi 21 ili kufanyika
uchaguzi mkuu mwingine, ni wazi ikitumika vizuri inaweza kuleta
mabadiliko makubwa kwenye jamii na kukijengea imani na kwenye chama
kikashinda Uchaguzi Mkuu 2015.
"Tunawaomba
Watanzania tuwape muda wateule hawa wa Rais watimize wajibu wao, lakini
tusisite kusema pale tutakapoona mambo hayaendi kama tunavyotarajia.
Uwajibikaji wa kweli ndio msingi wa mafanikio na maendeleo yetu,"
anasisitiza Nape.
HABARI LEO