

Hakika cheo ni dhamana, hivyo ni muhimu kwa
wenye dhamana hiyo kujitambua na kuonyesha wanavyoweza kubeba dhamana
hiyo kwa jamii husika.
Halima Dendegu, ambaye sasa ni Mkuu wa Wilaya ya
Tanga, mkoani Tanga anaweza kuwa mfano wa kuigwa kwa kuonyesha
alivyobeba dhamana hiyo ya kuiongoza wilaya kutokana na kugeukia kundi
la vijana wilayani kwake akidhamiria kuwakomboa.
Dendegu aliyeteuliwa na Rais Jakaya Kikwete, Mei
mwaka 2012 kuwa mkuu wa wilaya hiyo anaeleza kuwa baada ya kuingia
wilayani humo alifanya utafiti na kubaini kundi kubwa la vijana
likijihusisha na matumizi ya dawa za kulevya kwa sababu mbalimbali.
“Nilianza kubaini vijiwe vingi vya vijana na
hawana ajira, nilipofuatilia zaidi niligundua wengi wametumbukia katika
matumizi ya dawa za kulevya,”anasema Dendegu na kuongeza:
“Nilibaini vijana 867 wavulana na wasichana, walioathirika kwa matumizi ya dawa za kulevya.”
Anabainisha kuwa baada ya kuwahoji vijana hao
walitoa sababu mbalimbali za kujiingiza kwenye dawa za kulevya ikiwamo
kukosa ajira, makundi na kukata tama.
“Wengine walisema walishawishiwa, wapo waliosema
kiingiacho mjini siyo haramu, waliokuwa wakiuza dawa hizo, hata
walioshindwa kutimiza malengo yao maishani,” anasema Dendegu.
Anaongeza: “Kwa sababu hiyo, nimeanzisha kituo ili
kuwatibu, kimeanza na vijana 150 na 78 kati yao wameanza matibabu
wakiwamo wasichana 28.”
Anabainisha kwamba kwa kuwa lengo lake ni
kuwaepusha wasirudi kwenye dawa za kulevya katika kituo hicho ameanzisha
pia utoaji elimu ya ujasiriamali.
“Tayari tumebabini wenye vipaji mbalimbali, wapo
wapenda mpira wa miguu, watengenezaji sabuni hata wasanii wa muziki wa
kizazi kipya.”
Anasema kuwa ili kuwajenga zaidi kiafya na
kuanikiza vipaji vyao, kila Jumamosi huandaliwa bonanza linaloendana na
michezo mbalimbali.
“Pia nimeanzisha michuano ya mpira ‘Dendegu Cup’
litazinduliwa Juni mwaka huu ili kuibua vipaji zaidi, naamini tutatoa
vijana wa kucheza timu kubwa,”anasema akidokeza kuwa hata yeye anapenda
na kucheza mpira wa pete, volleyball, pia kuimba.