Kikwete: Tusaidieni kufunga masoko ya pembe za tembo


Rais Kikwete na mtoto wa malkia, Prince Charles

RAIS Jakaya Kikwete ameitaka Jumuia ya Kimataifa kusaidia kukomesha na kufunga masoko ya pembe za tembo na faru kama moja ya njia za kukomesha mauaji na biashara haramu ya wanyamapori hawa.

Akizungumza jana kwenye mkutano wa kimataifa wa kukabiliana na ujangili na biashara haramu ya pembe za tembo kwenye jumba la Lancaster jijini London, Uingereza, Rais Kikwete alisema kuwa bila kufunga masoko hayo kazi ya kudhibiti ujangili na mauaji ya wanyamapori hao itakuwa ngumu.
Rais Kikwete alikuwa mmoja wa viongozi wa Afrika ambao walizungumza kwenye ufunguzi wa mkutano huo uliohudhuriwa na wakuu wa serikali na nchi pamoja na wawakilishi wa nchi 60 duniani.
Mkutano huo umeandaliwa na Serikali ya Uingereza kwa ombi la mtoto wa malkia, Prince Charles.
Mbali na Rais Kikwete, viongozi wengine wa Afrika walioshiriki mkutano huo na kuzungumza ni pamoja na Rais wa Botswana, Jenerali Khama Iam Khama; Rais wa Gabon, Ali Omar Bongo na Rais wa Chad, Idrissa Deby. Ethiopia iliwakilishwa na waziri.
Rais Kikwete amewaambia mamia ya wajumbe wa mkutano huo: “Mwisho, nataka kuiomba jumuia ya kimataifa kuweka msimamo na kusaidia kukomesha biashara ya pembe za tembo na faru duniani. Kama hili litafanyika tembo na faru watakuwa salama.”
Ameongeza: “Wakati CITES ilipopiga marufuku biashara ya pembe za tembo mwaka 1989, hali hiyo ilisaidia kuongezeka kwa idadi ya tembo duniani. Naamini kuwa kama biashara hiyo itapigwa marufuku tena leo, matokeo yatakuwa yale yale. Maisha ya tembo na faru wengi yataokolewa na hatutakuwa na haja ya kuwa na wasiwasi.”
Rais Kikwete pia ametoa mapendekezo mengine makuu manne kama njia ya kukabiliana na ujangili na biashara haramu ya pembe za ndovu, ikiwa ni pamoja na ahadi kwamba serikali itaendelea kuongeza nguvukazi ya maofisa na askari wanyamapori na kuhakikisha kuwa maofisa na askari hao wanapata mafunzo mwafaka ya kuifanya kazi hiyo.
Wakati huo huo, Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) limeitaka Tanzania kuanzisha haraka awamu ya pili ya Operesheni Tokomeza yenye lengo la kukabiliana na kasi kubwa ya ujangili na mauaji ya wanyamapori katika Tanzania.
Shirika hilo limesema kuwa linatambua na kupongeza juhudi zinazofanywa na Serikali ya Tanzania kupambana na ujangili, ikiwa ni pamoja na kuanzisha Operesheni Tokomeza kupambana na balaa la uwindaji haramu wa wanyamapori na biashara haramu ya meno ya tembo.
Msimamo na pongezi hizo za UNDP zimetolewa juzi na Mkuu wa Shirika hilo la Umoja wa Mataifa, Hellen Clark wakati alipozungumza kwenye mkutano huo wa kimataifa wa kupambana na ujangili na biashara haramu ya meno ya tembo.
Katika hatua nyingine, Uingereza imemwalika Rais Kikwete kwa ziara rasmi kutembelea nchi hiyo kwenye sehemu ya kwanza ya mwaka huu, na amekubali mwaliko huo.
“Tunakualika rasmi na kukuomba Mheshimiwa Rais uwe mgeni wa Serikali ya Uingereza wakati wowote katika sehemu ya kwanza ya mwaka huu,” Waziri wa Mambo ya Nje na Jumuia ya Madola wa Uingereza, William Hague amemwambia Rais Kikwete ambaye naye ameukubali mwaliko huo.
Waziri Hague ametangaza hatua hiyo ya Uingereza kumwalika Rais Kikwete alipokutana na kufanya mazungumzo na waziri huyo kwenye makao makuu ya wizara hiyo jijini London.