MWANGWI
wa uamuzi wa Kamati Kuu ya Chadema wa kumvua madaraka aliyekuwa Naibu
Katibu Mkuu, Zitto Kabwe na wenzake, mbali na kutikisa katika kanda
sita kati ya kanda nane muhimu za chama hicho nchini, sasa umeanza
kukubalika na Sekretarieti ya chama hicho Taifa.
Jana
Kurugenzi ya Habari ya Chadema, ilituma ratiba ya ziara za Katibu Mkuu
wa Chadema, Dk Willibrod Slaa, mikoani iliyoonesha amekubali ushauri wa
kusogeza mbele ziara ya kutembelea majimbo nane ya Kigoma.
Awali
Dk Slaa alitarajiwa kuanza ziara ya kuimarisha chama mkoani Kigoma
kuanzia kesho lakini juzi Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Kigoma, Jafari
Kasisiko, alisema baada ya kutafakari kwa kina na kwa kutumia hekima na
busara, walipendekeza ziara hiyo isogezwe mbele...
Sababu
za mapendekezo hayo kwa mujibu wa Kasisiko, ni kutoa nafasi kwa uongozi
wa Mkoa, kwenda kuwaelimisha wanachama kutii uamuzi wa Kamati Kuu wa
kumvua madaraka Zitto na wenzake, hata kama uamuzi huo umewaudhi, lakini
lengo ni kudhibiti vitisho vya kuvuruga amani katika ziara hiyo
vilivyokuwa vimetolewa.
“Mkoa
uliomba Taifa liahirishe na kusogeza mbele tarehe ya ziara hiyo muhimu
kwa mkoa wetu, ili Mkoa kama ngazi ya chini ya Kanda na Taifa, uende
katika majimbo hayo na kuwaelimisha wanachama na wapenzi wetu, kuhusu
kuheshimu na kuwa na nidhamu na uamuzi utolewao na ngazi ya juu yetu,
hata kama una maumivu.
"Maoni ya wengi mkoani na kwa viongozi wa Chama ni kuudhiwa na uamuzi wa Kamati Kuu ambao ni dhahiri ulilenga kummaliza Zitto kisiasa.
"Maoni ya wengi mkoani na kwa viongozi wa Chama ni kuudhiwa na uamuzi wa Kamati Kuu ambao ni dhahiri ulilenga kummaliza Zitto kisiasa.
"Mkoa
ulitishika na vitisho baada ya kupokea taarifa kutoka kwa baadhi ya
viongozi wa majimbo ya Mkoa, kuwa hali ya usalama si nzuri kwa ujio wa
kiongozi wetu Dk Slaa… endapo hali haitokuwa salama Mungu aepushie
mbali,” alisema Kasisiko katika taarifa yake.
Dk Slaa ashaurika
Pamoja
na Chadema kusisitiza kuwa ziara hiyo itakuwepo, lakini taarifa ya jana
ya Kurugenzi ya Habari ya Chadema, ilieleza kuwa badala ya kuanza ziara
mkoani Kigoma kama ilivyokuwa awali, sasa ataanza ziara ya siku 20
kuanzia leo lakini mkoani Shinyanga.
Bila
kufafanua atakaa Shinyanga kwa siku ngapi, taarifa hiyo ilifafanua
kwamba ziara hiyo itamfikisha Dk Slaa mpaka mkoani Kigoma, ingawa
haikueleza lini atakwenda katika mkoa huo anakotoka Zitto na atakaa kwa
siku ngapi.
“Siku
ya Jumatano Desemba 4 mwaka huu (leo), Katibu Mkuu Dk Slaa atakuwa
Wilaya ya Kahama, siku inayofuata Desemba 5, atakuwa Wilaya ya Kakonko,
Jimbo la Buyungu na Desemba 6, atakuwa Jimbo la Muhambwe. Ratiba ya siku
zinazofuata itaendelea kutolewa kwa vyombo vya habari,” ilieleza
taarifa hiyo ya Kurugenzi ya Habari ya Chadema.