TAFAKURI JADIDI: Kagasheki
atauweza mfupa uliowashinda mawaziri wanne?
Makala ya Johnson Mbwambo katika gazeti la RAIA
MWEMA, Toleo la 248, Julai 11, 2012
Mbwambo

KUNA
Watanzania wameanza kusisimshwa na utendaji kazi wa Waziri Mpya wa Maliasili
na Utalii, Hamis Kagasheki. Asili ya kusisimshwa kwao ni namna alivyoanza
kazi mara baada ya kuteuliwa kuiongoza wizara hiyo badala ya Ezekiel Maige.
Siku chache tu baada ya kuingia ofisini, Waziri Kagasheki aliwashukia kwa
kishindo na kuwasimamisha kazi maofisa wanaotuhumiwa kuhusika na kuuawa kwa
faru wawili huko Serengeti.
Majuzi hapa Kagasheki alitema tena cheche nyingine alipowasimamisha maofisa
10 waandamizi katika wizara yake kupisha uchunguzi dhidi yao. Wakati
akiwasimamisha maofisa hao, Waziri Kagasheki alitangaza kuwa sasa ameanza
kazi rasmi kuisafisha wizara hiyo.
Hayo na mengine kadhaa ndio yanayowaaminisha baadhi ya Watanzania kwamba
wizara sasa imepata kiongozi mahiri, na mchapakazi kweli kweli.
Niseme mwanzoni kabisa kwamba mimi si mmoja wa hao wanaoamini kuwa wizara
sasa itatulia kwa sababu ipo chini ya
kamandoo
mahiri aliyepania kupambana na ufisadi uliokithiri katika wizara hiyo.
Nijuavyo mimi, na nikizingatia rekodi za nyuma, hatua hizi za sasa za
Kagasheki ni “nguvu za soda” tu; kwani hata mawaziri wengine wa wizara hiyo
waliomtangulia walianza hivyo hivyo!
Wote waliotangulia walitamba bungeni wakati wakiwasilisha bajeti zao kwamba
wataisafisha wizara hiyo, lakini hilo halikutokea, na waliishia kuhamishwa
wizara au kuenguliwa kabisa uwaziri.
Nina hakika Kagasheki naye atatamba hivyo hivyo wakati atakapowasilisha bajeti
yake, kwa mwaka wa fedha 2012/13, Jumatano ya Julai 11. Ni muda gani atadumu
katika wizara hiyo, ni suala la muda tu jibu litafahamika.
Kitakachomkwaza Waziri Kagasheki, na ambacho ndicho kilichowakwaza mawaziri
wenzake waliomtangulia, ni vigogo wenye ushawishi mkubwa nchini katika sekta
ya utalii na misitu. Hao ndio waliosababisha kung’atuliwa kwa mawaziri
waliomtangulia, na wa mwisho akiwa Ezekiel Maige.
Na kwa sababu vigogo hao bado wapo, na bado wana ushawishi mkubwa kwa
watawala wetu, ni vigumu kwa Waziri Kagasheki kukomesha ufisadi katika wizara
hiyo; hata kama atatimua maofisa wote wa ngazi za juu wa wizara hiyo na
kuweka wapya! Ilimradi vigogo hao wenye ushawishi mkubwa bado wapo, itakuwa
tu ni business as usual!
Uwepo wa mtandao huo wa vigogo wenye ushawishi mkubwa kwa watawala wetu
umethibitishwa karibu na mawaziri wote waliopitia wizara hiyo katika miaka ya
karibuni ya utawala wa Rais Kikwete; yaani kina Anthony Diallo,
Jumanne Maghembe, Ezekiel Maige, nikiwataja wachache.
Hebu tukumbushane ushuhuda wao tukianzia na Diallo. Huyu alipokuwa Waziri wa
Maliasili na Utalii, mwaka 2006, alitangaza kwamba biashara haramu ya uuzaji
magogo nje ya nchi ilikuwa ikifanywa na vigogo kadhaa wenye nguvu; huku
baadhi yao wakiwa serikalini.
Waziri huyo alibainisha kuwa, makampuni mengi yaliyosajiliwa yanayofanya
biashara haramu ya kuuza magogo nje ya nchi yanamilikiwa (kwa siri) na baadhi
ya viongozi waandamizi serikalini kwa kushirikiana na vigogo kadhaa.
Waziri Diallo hakupata kuyataja majina ya viongozi hao, lakini baadaye
aliondolewa katika wizara hiyo. Inaaminika kuondolewa kwake katika wizara
hiyo kulikuwa na ‘mkono’ wa mmoja wa vigogo hao wenye ushawishi mkubwa kwa
watawala wetu.
Ushuhuda mwingine wa uwepo wa vigogo hao wenye ushawishi mkubwa wanaokwamisha
juhudi za kumaliza ufisadi katika wizara hiyo, ulitolewa na Waziri Maghembe.
Baada ya kukaa katika wizara hiyo kwa muda mfupi tu, Waziri Maghembe naye
aliirudia kauli hiyo ya mwenzake kwamba wanaojihusisha na biashara hiyo
haramu ya magogo nchini, ni vigogo wenye ushawishi mkubwa nchini.
Kwa hakika, Waziri Maghembe yeye alikwenda mbali zaidi kwa kuliambia bunge
kwamba tayari alishamkabidhi Rais Kikwete orodha nzima ya vigogo hao. Mpaka
leo majina yaliyomo kwenye orodha hiyo ya Waziri Maghembe yamebakia kuwa siri
ya Ikulu!
Lakini ushuhuda wa hivi karibuni kabisa wa kuwepo kwa vigogo hao wenye
ushawishi mkubwa wanaokwamisha vita dhidi ya ufisadi katika wizara hiyo
ulitolewa na Ezekiel Maige mara baada ya kutemwa uwaziri.
Maige aliufahamisha umma kwamba vita dhidi ya ufisadi katika wizara hiyo
inakwamishwa na vigogo hao, na kwamba kung’olewa kwake kuwa waziri wa wizara
hiyo kunatokana na ushawishi wao; hasa baada ya kumuona ni kikwazo.
Maige alisema ya kuwa vigogo hao hawakufurahishwa na namna alivyolivalia
njuga suala la utoroshaji wanyama hai nje ya nchi au ugawaji mzuri wa vitalu
vya uwindaji, na hata udhibiti wa biashara haramu ya uuzaji magogo nje ya
nchi.
Tofauti pekee kati ya Maige na wenzake wawili – Maghembe na Diallo, ni kwamba
yeye aliweka mambo hadharani baada ya kuwa ametimuliwa uwaziri wakati wenzake
walitoboa siri hiyo wakati bado wakiwa mawaziri.
Vyovyote vile; tulichojifunza kutoka kwa ushuhuda wa mawaziri wote watatu ni
kwamba wanaokwamisha vita dhidi ya ufisadi katika wizara hiyo ni watu wenye
nguvu kubwa nchini ambao mawaziri hawana ‘ubavu’ wa kuwagusa.
Na ndio maana nasema kwamba; ilimradi vigogo hao bado wapo, ilimradi mtandao
wao bado upo, na ilimradi wanaendelea kukingiwa kifua na watawala wetu,
Waziri Kagasheki na juhudi zake za sasa ataishia tu kule kule walikoishia
wenzake waliomtangulia.
Lakini tumwonee huruma zaidi Waziri Kagasheki kwa sababu adui yake sasa
si vigogo hao tu; kwani ameongezeka adui wa pili katika biashara haramu ya
kuuza magogo nje ya nchi na pembe za wanyama - adui huyo mpya ni
Wachina!
Tangu Serikali ya China ilipoweka sheria kali kulinda misitu ya China mwaka
1998, viwanda vya nchi hiyo vimekuwa vikikimbilia bara la Afrika kupata
mahitaji yao makubwa ya mbao kwa njia haramu. Hivi sasa asilimia 60 ya magogo
yanayovunwa nchini kwa njia za haramu huishia China!
Asasi ya Uingereza inayojishughulisha na uchunguzi wa biashara haramu za
maliasili – Environmental Investigation Agency (EIA) imeeleza
katika ripoti yake kwamba, Wachina wanajishughulisha na biashara haramu za
pembe za ndovu, vifaru na pia magogo katika pwani ya Tanzania na Msumbiji;
hususan maeneo ya Cabo Delgado na Nampula.
EIA, ambayo kwa miaka 10 imekuwa ikifuatilia kiuchunguzi ushiriki wa
makampuni ya kichina katika biashara hizo haramu barani Afrika, inasema
kwamba, maofisa wa China hutumia watu wa kati katika biashara hizo, na kwamba
meli zao husafirisha kila mwaka shehena za magogo kupeleka China.
Lakini bila hata kurejea utafiti huo wa EIA, wengi wetu tunafahamu kuwa mara
nyingi baadhi ya Wachina wanaokuja nchini kwa ajili ya miradi ya ujenzi pia
hujihusisha na biashara haramu ya magogo na pembe za wanyama.
Na mara nyingi watawala wetu wanasita kuwanyooshea vidole au kuwatia mbaroni,
kwa sababu ya kubweteshwa na ‘misaada’ na ‘mikopo laini’ ya Serikali ya
China.
Na Wachina wanalijua hilo, na ndio maana hupendelea zaidi kujihusisha na
biashara hizo ovu katika nchi za Afrika ambazo mifumo yake ya uongozi si
imara zikiwemo DR Congo, Sudan na Zimbabwe.
Kwa hiyo, Waziri Kagasheki si tu kwamba atakwamishwa na vigogo hao wenye
ushawishi mkubwa katika juhudi zake za kukomesha utoroshaji wanyama hai nje
ya nchi, ugawaji kifisadi vitalu vya kuwindia wanyama au uuzaji haramu wa
magogo nje ya nchi, lakini pia itabidi apambane na mafisadi wapya wanaochangia
kuteketeza misitu yetu – Wachina!
Ni ugumu huu unaotufanya baadhi yetu tuwe na shaka kama kweli Waziri
Kagasheki atauweza mfupa uliowashinda wizarani hapo kina Maghembe, Diallo na
Maige.
Ni suala la muda tu tutajua kama naye zake zilikuwa ni nguvu za soda tu sawa
na ilivyokuwa kwa mawaziri waliomtangulia!
Tafakari
|